Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema amesema baadhi ya mawaziri wamekuwa wakaidi kufuata ushauri wa kisheria ambao amekuwa akiutoa na kwamba hicho ndicho chanzo cha matatizo yote yanayotokea katika utendaji wa Serikali, yakiwamo yale yaliyobainika katika Ripoti ya Operesheni Tokomeza Ujangili.
Wakati Jaji Werema akiwananga mawaziri, kwa upande
mwingine amemsifia Rais Jakaya Kikwete akisema kuwa yeye si kama
mawaziri wake kwani ni msikivu na anayeshaurika. Akizungumza na
mwandishi wetu jana, Jaji Werema alisema endapo ushauri ambao amekuwa
akiutoa mara kadhaa kwa mawaziri ungezingatiwa, kilichotokea bungeni
mwishoni mwa wiki cha mawaziri kung’oka kisingekuwapo.
“Tunatakiwa kuiga msemo wa Mkuu wa Jeshi la
Polisi, Said Mwema kuwa ‘tii sheria bila shuruti’, Rais tunamshauri na
anashaurika kwa nini mawaziri wakatae kuzingatia ushauri?” alisema
Werema na kuongeza:
“Mawaziri hawatakiwi kujifanyia tu mambo yao.
Tunawaandikia barua lakini zinakwenda na yanafanyika yaleyale... Hata
mimi nikionekana kukiuka sheria na kanuni naweza kuwajibishwa kwa kuwa
hakuna aliye juu ya sheria.”
Jaji Werema alisema watu wanaweza kutofautiana
kisiasa lakini katika mambo yanayohusu haki za binadamu lazima
kuunganisha nguvu pamoja ili kuhakikisha sheria za nchi zinafuatwa bila
kupindishwa.
Alikuwa akizungumzia kuhusu kung’oka kwa mawaziri
wanne kutokana na matokeo ya uchunguzi wa Operesheni Tokomeza Ujangili
ambao ulifanywa na Kamati ya Bunge ya Maliasili na Mazingira.
Ripoti ya Kamati hiyo ilisababisha Rais Kikwete
kutengua uteuzi wa Mawaziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi
Vuai Nahodha, Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi, Maendeleo ya
Mifugo na Uvuvi, Dk Mathayo David Mathayo na Maliasili na Utalii, Balozi
Khamis Kagasheki.
Tume ya Kimahakama
Kadhalika, Jaji Werema alisema Tume ya Kimahakama
itakayochunguza kwa kina madhara yaliyojitokeza katika Operesheni
Tokomeza Ujangili iliyosababisha vifo, majeraha, utesaji wa kinyama,
uharibifu wa mali na upotevu wa mifugo, itaundwa na Rais Kikwete.
“Tume hii itakwenda mbali zaidi ya taarifa ya
kamati, itachunguza waliohusika, waliosemwa katika ripoti kwa juujuu
watatafutwa, kuangalia matumizi ya nguvu kiasi hicho na mwisho
mapendekezo ya tume hiyo juu ya kipi kifanyike kwa wahusika
itazingatiwa,” alisema na kuongeza:
“Hawa Mawakili wa Serikali waliokuwa katika
operesheni hiyo, DPP (Mkurugenzi wa Mashtaka) atatakiwa kutoa maelezo,
hao mawakili wake walikwenda huko kwa misingi gani pamoja na mahakimu
waliokuwa huko.”
Hata hivyo, Jaji mstaafu, Thomas Mihayo alisema
hakuna haja ya kuundwa kwa tume hiyo na kinachotakiwa ni kutumika kwa
sheria ya kutafiti sababu za vifo.
Alisema sheria hiyo ikitumika, wananchi watakwenda kutoa ushahidi mahakamani na wahusika kuchukuliwa hatua.
“Sijajua kwa nini sheria hii haitumiki hapa
nchini, sisi tuliitumia mwaka 1972 baada ya kumtia hatiani aliyekuwa
Mkuu wa Jeshi la Polisi, Hamza Azizi kwa gari lake kusababisha kifo,”
alisema na kuongeza:
“Nafikiri ataiunda mkuu wa nchi na ripoti
kukabidhiwa kwake kwani waziri mkuu hawezi kukabidhiwa kutokana na kile
kilichotokea bungeni kuwa ameshindwa kusimamia mawaziri wake.”
Kauli ya Jaji Mihayo iliungwa mkono na mtazamo wa
Profesa Issa Shivji ambaye alisema watendaji, wakiwamo wa ngazi za juu,
wafikishwe mbele ya mahakama kwa mashtaka ya kijinai.
“Mwanasheria Mkuu amependekeza uundaji wa tume ya
kimahakama. Hii ni njia moja wapo lakini mara nyingi njia hii hutumika
kama mbinu za kufunika kombe ili mwanaharamu apite,” alisema Profesa
Shivji katika makala yake ambayo imechapishwa katika gazeti hili.
Aliongeza: “Nionavyo, labda safari hii, Rais Kikwete anaweza kutumia
njia mbadala ya kuteua mchunguzi huru ambaye atakusanya ushahidi na
kuandaa mashtaka ya kupeleka mbele ya Mahakama.”
Alisema katika uchunguzi huo, watendaji wote
wanaohusika, pamoja na wa kijeshi, usalama na wa kiraia, wachunguzwe na
kushtakiwa bila kujali nyadhifa zao.
Msajili wa Vyama vya Siasa Mstaafu, John Tendwa
alisema lengo la kuundwa kwa tume hiyo ni kuchunguza jambo fulani kwa
kina ili kubaini chanzo na hatua za kuchukuliwa kwa wahusika huku ikiwa
chini ya mwenyekiti ambaye ni jaji.
Tendwa alisema tume hiyo inaweza kushirikisha watu kutoka sehemu tofauti mbali na mahakama.
“Inakuwa chini ya jaji ili kuhakikisha haki
inatendeka na si lazima wawe majaji watatu au wangapi lakini inajumuisha
pia watu kutoka kada tofauti ndani ya mfumo wa kimahakama ili
kuchunguza kwa undani tukio fulani,” alisema Tendwa.
CHANZO GAZETI MWANANCHI
CHANZO GAZETI MWANANCHI
0 comments:
Post a Comment