KIONGOZI wa Kambi ya Upinzani Bungeni, 
Freeman Mbowe, amepongeza msimamo wa wabunge hasa wa CCM kwa kuweka 
itikadi zao pembeni na kusimamia kidete suala la bajeti ya Wizara ya 
Maji, hadi ikasitishwa ili iboreshwe zaidi. Pia kiongozi huyo, pamoja na
 kudai kuwa adhabu waliyopewa wabunge watano wa chama chake 
haikustahili, lakini akakiri kuwa walihusika katika vurugu ndani ya 
Bunge, ikiwa ni pamoja na mmoja wao kudharau mamlaka ya Spika.
Aidha, Mbowe amebainisha kuwa kambi ya 
upinzani inataka utaratibu wa mashine za kupigia kura zilizopo ukumbini 
kwenye kila meza ya mbunge uanze kutumika mara moja, badala ya kura za 
ndiyo na hapana ili kuondokana na mikanganyiko na kutotendeka kwa haki 
wakati wa kupiga kura hizo.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini dodoma, Mbowe alisema mshikamano uliojionesha wa wabunge bila kujali
 itikadi zao za vyama wakati wa kujadili bajeti ya maji umeonesha 
ukomavu wa kisiasa, hali ambayo ndiyo inapaswa iendelezwe bungeni.
“Nashukuru jana (juzi) bungeni wabunge 
wengi wakiwamo wa CCM walikataa kuiunga mkono hoja hii ya bajeti kwa 
msingi mmoja, kwamba haikidhi mahitaji, na sisi wapinzani kwa kweli hoja
 zetu zilipata nguvu kwa sababu takribani wabunge wote walituunga 
mkono,” alisema.
Alisema endapo kila siku hali ya 
uchangiaji na misimamo ya maslahi ya Taifa itafanyika kama ilivyofanyika
 katika hoja ya maji, ni wazi kuwa ushirikiano wa aina hiyo utaijenga 
nchi kwa misingi ya maendeleo.
Hata hivyo, Mbowe alitaka Wizara ya 
Maji, keshokutwa itakapowasilisha maboresho hayo katika bajeti yake, ije
 na mipango thabiti ya kumaliza tatizo la maji nchini, ikiwa ni pamoja 
na kuachana na kutafuta Sh bilioni 100 za kuongezewa katika bajeti hiyo 
na kutafuta zaidi ya Sh bilioni 500 ili kutekeleza Mpango wa Maendeleo 
wa Miaka Mitano.
Kuhusu adhabu za wabunge watano wa chama
 chake kupewa adhabu kwa utovu wa nidhamu, alikiri kuwa mmoja wa wabunge
 wa chama chake, alidharau mamlaka ya Spika lakini kanuni zilizotumika 
hazikustahili na zilikuwa kiini macho.
Alisema Naibu Spika, Job Ndugai, 
hakustahili kutumia kanuni hizo za kifungu cha 2.2 na 5 za Bunge toleo 
la mwaka 2013, ambazo zinamtaka Spika atoe uamuzi kuhusu jambo 
litakalotokea bungeni endapo katika kanuni zilizopo hazina Mwongozo.
“Ukweli ni kwamba vurugu zilizotokea 
bungeni na kitendo cha mbunge wetu Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Tundu 
Lissu kinachodaiwa kuwa amedharau mamlaka ya kiti, kanuni zake zipo 
pamoja na adhabu yake,” alisema.
Alisema katika kanuni hizo za Bunge, 
vifungu 74 na 76 zimebainisha wazi adhabu zinazotakiwa kutolewa kwa 
mbunge atakayebainika kudharau mamlaka ya Spika au kuwa chanzo cha 
vurugu ndani ya Bunge.
“Ni kweli hakuna shaka kabisa mbunge 
wetu alidharau mamlaka ya Spika, lakini zipo adhabu stahiki za 
kushughulikia suala hilo, na kwa namna kanuni hizo zilivyo kama 
zingetumika vizuri, huenda adhabu ingekuwa kubwa zaidi ya hii 
iliyotolewa, huku akiongeza kuwa wabunge hao walioadhibiwa hawakupewa 
haki ya kusikilizwa,” alisisitiza.
Adhabu hizo ni pamoja na Spika kutaja 
jina la Mbunge husika hadharani kuwa amedharau kiti na kumpeleka mbele 
ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka na Bunge na kwa upande wa fujo 
zinapotokea ndani ya ukumbi huo wa Bunge, kabla ya kutoa hoja ya nguvu, 
hutakiwa kwanza kuahirisha Bunge.
“Siku ile kweli vurugu zilitokea na 
kulikuwepo na vitendo vya kudharau mamlaka ya Spika, lakini Naibu Spika 
alitakiwa kwanza aahirishe Bunge, ndipo atumie nguvu, sasa badala yake 
waliingia askari wa kila aina ndani ya ukumbi jambo ambalo ni kinyume na
 Kanuni za Bunge,” alisisitiza.
Aidha, alisema kuhusu suala la adhabu 
kwa mbunge anayedharau kiti au kuhusika na vurugu, hutakiwa kwanza Spika
 amfikishe mbunge husika mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka 
ambayo baada ya kushauriana ndipo hutoa adhabu ambayo ni kutohudhuria 
Bunge vikao 10 iwapo kosa ni la kwanza na vikao 20 iwapo kosa ni la 
pili.
“Adhabu yoyote inayotolewa bungeni 
hutolewa kwanza na Azimio la Bunge na si Spika mwenyewe, endapo kanuni 
zilizopo zingefuatwa, huenda wahusika kama wangethibitika kabisa kuwa 
wamekosa, wangepata adhabu kali zaidi kama zilivyoainishwa kwenye 
kanuni,” alisema Mbowe.
Wabunge wa Chadema walioadhibiwa 
kutokana na vurugu zilizotokea bungeni humo hivi karibuni pamoja na 
Lissu, ni Ezekiah Wenje (Nyamagana), Highness Kiwia (Ilemela), Joseph 
Mbilinyi (Mbeya Mjini), Godbless Lema (Arusha Mjini) na Peter Msigwa 
(Iringa Mjini).
Akizungumzia suala la mashine za kura 
bungeni, alisema utaratibu unaotumika sasa wa kura za ndiyo na hapana ni
 wa zamani na hautendi haki, kwani huegemea zaidi katika uamuzi wa Spika
 na si wabunge.
“Lakini Bunge letu lina vifaa 
vinavyoonesha namna ya kupiga kura na kuonekana kwenye meza ya Spika, 
tena yapo maelekezo yanayomwezesha mbunge husika jina lake lionekane au 
la, sasa sielewi kwa nini bado tunang’ang’ania mfumo wa ndiyo na hapana,
 hapa kuna mchezo mchafu,” alisisitiza.
Alisema mfumo huo ukitumika, utaongeza 
uhuru wa wabunge kupiga kura bila kujali itikadi za vyama na kutanguliza
 maendeleo ya wananchi, kwani kwa sasa mtindo wa kura za ndiyo na hapana
 hufanya wabunge wengine washindwe kutoa uamuzi sahihi kwa hofu ya 
kuitwa wasaliti.
Pamoja na hayo, Mbowe alisema kambi ya 
upinzani inaitaka Serikali iwasilishe utekelezaji wa maazimio kuhusu 
suala la Richmond, ripoti ya Jairo, maazimio ya kamati ndogo ya 
Maliasili na Utalii kuhusu usafirishaji wa twiga na wanyama wengine hai 
na suala la mabilioni ya Uswisi.
habari leo chanzo 





0 comments:
Post a Comment