Mtihani
wa uwakala wa wachezaji (players agent) na uwakala wa mechi (match
agent) wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) utafanyika
Alhamisi ya Septemba 26 mwaka huu saa 4 kamili asubuhi kwenye ofisi za
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
Kutakuwa
na jumla ya maswali 20 kwenye mtihani huo, 15 yanatoka FIFA kuhusiana
na kanuni za kimataifa za mpira wa miguu na matano yatatoka TFF
kuhusiana na kanuni mbalimbali zinazotawala mchezo huo nchini.
Kwa
ambao wangependa kufanya mtihani huo utakaokuwa katika lugha ya
Kiingereza ambayo ni moja kati ya lugha nne rasmi za FIFA wanatakiwa
kujisajili TFF kwa ada ya dola 50 za Marekani ambapo watapewa utaratibu
na maeneo ambapo mtihani huo unalenga.
Mtihani huo utafanyika saa 4 kamili asubuhi, na muda wa kufanya mtihani hautazidi dakika 90.
Mpaka
sasa Tanzania ina mawakala watano wa wachezaji wanaotambuliwa na FIFA.
Mawakala hao ni John Ndumbaro, Mehdi Remtulla, Ally Saleh, Yusuf
Bakhresa na Said Tully.
WAAMUZI VPL KUFANYA MTIHANI WA UTIMAMU WA MWILI
Waamuzi
wote wa daraja la kwanza (Class I) wanaotaka kuchezesha Ligi Kuu ya
Vodacom (VPL) msimu wa 2013/2014 wanatakiwa kuhudhuria mtihani wa
utimamu wa mwili (physical fitness test) utakaofanyika katika vituo
viwili.
Mtihani
huo utafanyika Agosti 12,13 na14 mwaka huu katika vituo vya Dar es
Salaam na Morogoro. Kituo cha Mwanza kitahusisha waamuzi kutoka mikoa ya
Geita, Kagera, Katavi, Kigoma, Manyara, Mara, Mwanza, Shinyanga,
Simiyu, Singida na Tabora.
Kituo
cha Dar es Salaam kitahusisha waamuzi kutoka mikoa ya Arusha, Dar es
Salaam, Dodoma, Iringa, Kilimanjaro, Lindi, Mbeya, Morogoro, Mtwara,
Njombe, Pwani, Ruvuma na Tanga.
Washiriki
wote wanakumbushwa kuwa ni lazima wafuate utaratibu huo wa vituo, na si
vinginevyo. Pia waamuzi waliofungiwa (sio maisha) wanatakiwa kushiriki
katika mtihani huo.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
0 comments:
Post a Comment