Main Menu

Tuesday, June 4, 2013

JWTZ YAKANUSHA VIKALI UJUMBE NA TETESI ZA KURUSHWA MABOMU KUTOKA MALAWI


Picture
JESHI LA ULINZI LA WANANCHI WA TANZANIA

Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limepata ujumbe  kupitia simu za mkononi ambao umesambazwa kwa wananchi mbalimbali ukisadikishwa kuwa unatolewa na JWTZ.

Ujumbe huo wa simu ya mkononi unasema ‘Habari zilizotufikia hivi punde. Mtanzania yeyote, kaa makini usiokote kitu chochote ambacho una shaka nacho, kuna bomu zimerushwa toka nchi jirani Malawi zaidi ya 30 zenye uzito usiopungua tani 100. Hivyo basi uonapo kitu kipo kama chupa la chai chenye rangi ya fedha. Usiguse’
 Piga namba 0756 000042. SMS hii tuma kwa watu uwezavyo. Imetolewa na JWTZ’.

JWTZ linapenda kuwaondoa wananchi hofu kutokana na taarifa hiyo. Kwanza, Ujumbe huo haujatolewa na
 JWTZ. JWTZ  haliwezi likatumia mfumo huo wa SMS kuwapa wananchi wake taarifa za hatari kama hizo. Aidha, JWTZ hutangaza kupitia vyombo rasmi kama vile Magazeti, Radio na Television.

Pili, bomu la tani 100 ni zito mno,  halijawahi kutengenezwa duniani. Na kama lipo, haifahamiki bomu hilo litarushwa vipi , kwa kutumia ndege au Mzinga?.  Lakini pia, mzinga wa aina hiyo haupo duniani kote na wala hakuna ndege yenye uwezo huo, hasa kwa bomu lenye umbile dogo kama hilo(Chupa ya Chai).

Tatu, habari hizi hazina ukweli kisayansi wala kiuhalisia au fikra za kawaida. Tunawaomba wananchi wazipuuzie taarifa hizi kwani sio za kweli ni uongo mtupu. JWTZ lipo kwa ajili ya Wanachi hivyo, kwa taarifa hizi za hatari,lazima lingewajulisha wananchi kwa njia zilizoelezwa hapo juu na si kwa simu za mkononi.



Imetolewa na Kurugenzi ya Habari na Uhusiano
Makao Makuu ya Jeshi, Upanga
SLP 9203, Simu: 0764-742161
Email:ulinzimagazine@yahoo.co.uk


0 comments:

Post a Comment