Main Menu

Friday, March 27, 2015

VILABU MBALIMBALI VYA LIGI KUU VYAPIGWA FAINI...........



Kikao cha Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania  kilichoketi jumanne ya tarehe 24, Machi 2015 jijini Dar es salaam, kimepitia taarifa mbalimbali za michezo iliyochezwa na kutoa adhabu kwa wachezaji na vilabu vya Ligi Kuu ya Vodacom.

Katika mechi namba 107 iliyowakutanisha wenyeji Ndanda FC dhidi ya Coastal Unioni, klabu ya Ndanda imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 42(1) ya Ligi Kuu ya Vodacom  kutokana na washabiki wake kumrushia chupa za maji mwamuzi msaidizi Anold Bugado.

Mechi namba 108 iliyochezwa Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, (Stand United dhidi Simba SC), wenyeji timu ya Stand United imepigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) kwa mujibu wa Kanuni ya 14(8) kutokana na timu yake kuchelewa kufika uwanjani kwa dakika ishirini.

Mchezo namba 117 uliozikutanisha Simba SC dhidi ya Yanga SC kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, timu ya  Simba imepigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) kwa mujibu wa Kanuni ya 14(9) kwa kukataa kuingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo.

Nayo klabu ya Yanga imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 42(11) baada ya timu yake kuonyeshwa kadi zaidi ya tano kwenye mchezo dhidi ya Simba SC, huku mshambualiji wake Dany Mrwanda  akipigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 14(12) kwa kutopeana mikono na wachezaji wa timu hiyo.

Mchezaji Haruna Niyonzima wa Yanga amepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 37(f) kwa kupiga teke meza ya   mwamuzi wa akiba baada ya kutolewa nje kwa kadi nyekundu. Suala la mshambuliaji wa Yanga Amissi Tambwe kumshika korodani beki wa Simba SC Murshid Juuko limepelekwa kwenye Kamati ya Nidhamu.
Kipa wa timu ya Simba SC, Ivo Mapunda amepewa onyo kwa kufunika tangazo la mdhamini wa Ligi Kuu  (Vodacom) kwa kutumia taulo lake wakati wa mechi dhidi ya Yanga, hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake iwapo atarudia kufanya tukio la aina hiyo.

Nao wachezaji Salum Abubakar wa Azam FC na Richard Maranya wa JKT Ruvu wamepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kila mmoja na kusimamishwa mechi tatu kwa mujibu wa Kanuni ya 37(3) kwa kupigana uwanjani kwenye mechi namba 123 ambapo walitolewa nje kwa kadi nyekundu.

Klabu ya Kagera Sugar imepigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) kwa mujibu wa Kanuni ya 14(9) baada ya timu yake kugoma kuingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo kwenye mchezo namba 130 dhidi ya Young Africans uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa.

Mechi namba 132 iliyozikutanisha Azam na Ndanda SC kwenye uwanja wa Chamazi, klabu ya Ndanda imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 42(1) baada ya washabiki wake kuwamwagia maji na kuwarushia chupa za maji washabiki wa Azam.

Aidha klabu ya Stand United imepigwa faini ya sh. 300,000 (laki tatu) kwa mujibu wa Kanuni ya 14(8) kwa kuchelewa kufika uwanjani kwenye mechi namba 134 dhidi ya timu ya Mbeya City,  pia imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 14(9) kwa kutoingia kwenye vyumba vya kubadilishia nguo kwenye mchezo huo.

Kiongozi wa Stand United, Muhibu Kanu amepelekwa kwenye Kamati ya Nidhamu baada ya kuondolewa kwenye benchi na mwamuzi wa mchezo dhidi ya Mbeya City kutokana na kutumia lugha ya kuhamasisha vurugu kwa timu yake na kupinga uamuzi wa refarii.

Katika mchezo namba 135 uliochezwa jijini Tanga na kuwakutanisha wenyeji Mgambo Shooting dhidi ya Yanga SC, Yanga SC imepigwa faini ya sh. 500,000 (laki tano) kwa mujibu wa Kanuni ya 42(1) kutokana na washabiki wake kuvamia uwanja baada ya mechi namba 135 dhidi ya Mgambo Shooting kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

0 comments:

Post a Comment