Main Menu

Thursday, August 1, 2013

MKEMIA MKUU: MAFUTA YA UBUYU HATARI KWA AFYA

Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samwel Manyele amewataka Watanzania kuacha kutumia mafuta ya ubuyu kwa maelezo kuwa yana kemikali yenye madhara kwa afya ya binadamu.

 
Manyele ameipinga kauli iliyotolewa na Taasisi ya Saratani ya Ocean Road mwanzoni mwa wiki hii kwamba mafuta hayo hayana madhara katika mwili wa binadamu yakitumiwa vizuri.

Juzi, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid, alitangaza kuwa mafuta hayo si salama na kusisitiza kuwa huo ndiyo msimamo wa Serikali kuhusu mafuta hayo, hivyo wananchi waamue wenyewe kuyatumia au kutokuyatumia.

Akizungumza na gazeti hili jana, Profesa Manyele alisema, “ Ofisi yangu inaiunga mkono kauli ya Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA) kuzuia matumizi ya mafuta hayo, Watanzania wanatakiwa kuwa wasikivu na onyo hilo.”

Alisema sheria inayoruhusu mtu yoyote kufanya biashara ya chakula na dawa ipo chini ya TFDA, wao ndio wanaotoa kibali cha kufanya biashara na kutengeneza bidhaa, kwamba wakisema bidhaa fulani haifai wanatakiwa kusikilizwa.

“Wao ndio wanaotoa kibali cha kutengeneza bidhaa, pia wana uwezo wa kuzuia uzalishaji kwa mujibu wa sheria. Ofisi ya Mkemia Mkuu haiwezi kuzuia uzalishaji,” alisema

Alisema tayari TFDA imeshaeleza athari ya kemikali iliyopo katika mafuta ya ubuyu inayoweza kuathiri afya ya Watanzania, kuwataka wananchi kuwa makini na kama wanahitaji taarifa za msingi wanatakiwa kwenda katika ofisi za Mamlaka hiyo.

“Mimi kama Mkemia Mkuu wa Serikali nitaingilia kati kama mambo yote yatashindikana na Serikali itataka kutoa tamko rasmi kuhusu matumizi ya mafuta haya,” alisema

Hivi karibuni, TFDA ilipiga marufuku matumizi ya mafuta ya ubuyu kwa madai kuwa yanasababisha saratani, tamko ambalo lilipingwa vikali na wataalamu wa tiba mbadala.

Daktari Bingwa wa Udhibiti wa Saratani, katika taasisi ya Ocean Road, Dk Crispin Kahesa juzi alizungumza na gazeti moja la kila siku (sio Mwananchi) mafuta hayo ni salama kwa matumizi ya binadamu, kama yakitumiwa vizuri.

Alisema mafuta ya ubuyu siyo dawa bali yanazuia maradhi sugu yasiyoambukiza, yakiwamo saratani kwa sababu kitaalamu yana ‘ant oxidant’ (uchachu) ambao pia hupatikana kwenye baadhi ya matunda kama maembe, machungwa na mananasi.

Kitendo cha Taasisi ya Saratani ya Ocean Road kutangaza kuwa mafuta hayo ni salama iwapo yakitumiwa vizuri, pamoja na mwendelezo wa malalamiko kutoka kwa wananchi na wataalamu mbalimbali, limekuwa likizua utata kwa kuwa kila upande unaonekana kutoa msimamo wake jambo ambalo limeibua mjadala katika jamii.
Tamko TFDA
TFDA ilitoa taarifa kuhusu matumizi ya mafuta ya ubuyu na kueleza kuwa yana kiwango kikubwa cha tindikali ya mafuta aina ya cyclopropenoic fatty acids ambayo huweza kusababisha athari ya kiafya endapo mafuta hayo yatatumika kama chakula.

Ilieleza kuwa kiwango cha tindikali hiyo huweza tu kupunguzwa katika mafuta ya mbegu za ubuyu kwa kuchemsha mafuta hayo katika nyuzi joto 180 kwa muda wa saa nane au kwa kutumia teknolojia ya kutengeneza mafuta mgando (hydrogenation).

“Kwa sasa hapa nchini hakuna aina ya usindikaji unaofanyika wenye uwezo wa kuondoa tindikali ya cyclopropenoic fatty acids katika mafuta ya mbegu za ubuyu” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Ilieleza kwamba baadhi ya athari zinazoweza kutokana na matumizi ya mafuta ya ubuyu ni pamoja na kuathiri vimeng’enyo (enzymes) vinavyosaidia katika uchakataji wa tindikali za mafuta mwilini (fatty acid biosynthesis).

NA gazeti mwananchi.

0 comments:

Post a Comment