Main Menu

Thursday, December 27, 2012

WANANCHI MKOANI MTWARA WAANDAMANA KUPINGA GESI KUPELEKWA JDAR ES SALAAM

Maelfu ya wakazi wa mkoa wa Mtwara na vitongoji vyake leo wamefanya maandamano ya amani wakipinga mpango wa serikali ya Tanzania wa kusafirisha gesi asilia iliyoko mkoani humo kwa kutumia mabomba hadi Dar es Salaam. 

Waandamanaji hao wakiwa wamebeba mabango yenye kuelezea jumbe na hisia zao, wameanza maandamano hayo asubuhi  katika maeneo ya Mtawanya na kuelekea Mtwara mjini. 

Madai ya wananchi wa Mtwara ni pamoja na kutaka gesi hiyo asilia isipelekwe moja kwa moja hadi Dar es Salaam, kijengwe kiwanda cha gesi na wenyeji wapewe kipaumbele katika ajira na makampuni ya kuchimba gesi yatoe huduma za kijami kama vile maji, afya, elimu na barabara katika maeneo husika. 

Taarifa zinasema kuwa, kinyume na maandamano yaliyowahi kufanyika katika mikoa mbalimbali hivi karibuni nchini humo, maandamano ya wananchi wa Mtwara hayakugubikwa na ghasia wala machafuko, ingawa askari polisi walitanda pambizoni mwa waandamanaji  ili kuhakikisha  unakuwepo usalama wa wananchi na mali zao. 

Wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara kwa miaka kadhaa wamekuwa wakilalamika kwamba, mikoa hiyo iko nyuma kimaendeleo kulinganisha na mikoa mingine. 

Rais Jakaya Kikwete  alizindua rasmi ujenzi wa bomba hilo Novemba 8, mwaka huu katika eneo la Kinyerezi jijini Dar es Salaam.

chanzo, idhaa ya kiswahili radio tehrani

0 comments:

Post a Comment